Mkuu wa jeshi la Sudan Kusini awapa wanajeshi siku saba kumaliza uasi
https://parstoday.ir/sw/news/africa-i135862-mkuu_wa_jeshi_la_sudan_kusini_awapa_wanajeshi_siku_saba_kumaliza_uasi
Mkuu wa majeshi ya Sudan Kusini amewapa wanajeshi muda wa siku saba “kuukandamiza uasi” mashariki mwa nchi, ambao unatishia usalama wa mji mkuu, Juba.
(last modified 2026-01-25T00:41:24+00:00 )
Jan 25, 2026 00:41 UTC
  • Mkuu wa jeshi la Sudan Kusini awapa wanajeshi siku saba kumaliza uasi

Mkuu wa majeshi ya Sudan Kusini amewapa wanajeshi muda wa siku saba “kuukandamiza uasi” mashariki mwa nchi, ambao unatishia usalama wa mji mkuu, Juba.

Hivi karibuni, Jeshi la Ukombozi wa Watu wa Sudan kwa Upinzani (SPLA-IO) lilivamia na kuteka maeneo kadhaa katika jimbo la Jonglei, kwa mujibu wa mwandishi wa habari wa eneo hilo aliyeliambia BBC, ingawa taarifa hizo hazikuweza kuthibitishwa kwa njia huru.

Mapigano ya hivi karibuni yameutishia mji mkuu wa Jonglei, Bor, ulioko umbali wa takribani saa mbili kwa gari kutoka mji mkuu Juba.

Kiongozi wa SPLA-IO, Makamu wa Kwanza wa Rais aliyesimamishwa kazi, Riek Machar, kwa sasa yuko mahakamani akikabiliwa na mashtaka ya mauaji, uhaini na uhalifu dhidi ya ubinadamu, ambayo ameyakanusha.

Kuna hofu kwamba mapigano haya yanaweza kuchochea tena vita kamili vya wenyewe kwa wenyewe katika nchi hiyo change zaidi barani Afrika.

Vikosi vya ziada vya jeshi la Sudan Kusini sasa vimetumwa mjini Bor, ambao ulikuwa mji wa kwanza kutekwa na majeshi ya upinzani katika mgogoro wa miaka 2013–2018. Mji huo unaonekana kuwa kituo muhimu cha kimkakati kuelekea mji mkuu.

“Tuliwaleta hapa kwa ajili ya ujumbe maalum,” alisema mkuu wa majeshi ya ulinzi, Jenerali Paul Nang Majok, akiwaambia wanajeshi wake.

“Ninawapa siku saba tu kukamilisha hilo, kuwamaliza waasi katika maeneo hayo na kuyarejesha chini ya udhibiti wetu.”

Jeshi la Sudan Kusini linaungwa mkono na wanajeshi kutoka Uganda. Idadi yao halisi haijulikani. Ripoti moja imetaja idadi ya wanajeshi 4,000, lakini taarifa hiyo haijathibitishwa.