Tanzania: Kesi ya uhaini ya Tundu Lissu inaendelea tena leo
-
Tanzania: Kesi ya uhaini ya Tundu Lissu inaendelea tena leo
Mahakama Kuu ya Tanzania imepanga kuendelea tena kesi ya uhaini inayomkabili kiongozi wa upinzani Tundu Lissu. Ripoti zinasema, kesi hiyo inaendelea leo Jumatatu Februari 9 hadi Machi 6, 2026, mbele ya Mahakama Kuu jijini Dar es Salaam.
Kulingana na Gaston Garubindi, mkurugenzi wa masuala ya sheria wa chama cha upinzani cha CHADEMA, kesi hiyo, iliyosajiliwa chini ya nambari 19605/2025, inasikilizwa na jopo la majaji watatu: D. Ndunguru, J. Karayemaha, na Kiwonde.
Garubindi alithibitisha kwamba Lissu, mwenyekiti taifa wa chama cha upinzani CHADEMA, alipokea taarifa rasmi kutoka kwa Naibu Msajili wa Mahakama Kuu mnamo Januari 14, 2026. Lissu alikamatwa Aprili 9, 2025, wakati wa mkutano huko Mbinga, Mkoa wa Ruvuma, na alikuwa amezuiliwa kwa siku 282 kufikia Januari 15, 2026.
Ikumbukwe kuwa, kesi hiyo kwa sasa ipo kwenye hatua ya mashahidi wa Jamhuri kuendelea kutoa ushahidi wao Mahakamani hapo, hata hivyo mara ya mwisho kutajwa Mahakamani, mshtakiwa (Tundu Lissu) ambaye anajitetea mwenyewe aliwasilisha mapingamizi kadhaa ambayo bila shaka leo upande wa Jamhuri wataanza kwa kuyajibu.
Tundu Lissu ambaye ni Mwenyekiti Taifa wa chama cha uopinzani nchini Tanzania cha Demokrasia na Maendeleo CHADEMA amepandishwa kizimbani mara kadha kwa tuhuma za uhaini; shitaka ambalo hukumu yake ni kifo, kwa matamshi yake aliyoyatoa ambayo waendesha mashtaka walisema alitoa wito kwa umma kuanzisha uasi na kuvuruga uchaguzi.