UN yaunga mkono juhudi za kuwarejesha nyumbani wakimbizi CAR
Umoja wa Mataifa umetangaza uungaji mkono wake kwa juhudi za kuwarejesha nyumbani wakimbizi wa Jamhuri ya Afrika ya Kati.
Mtandao wa habari wa Africa Time umemnukuu Kouassi Lazare Etien, mjumbe wa Shirika la Wakimbizi la Umoja wa Mataifa UNHCR akisema mbele ya waandishi wa habari, mwishoni mwa ziara yake huko Bangui, mji mkuu wa Jamhuri ya Afrika ya Kati kuwa, Umoja wa Mataifa unaunga mkono suala la kurejea kwa hiari wakimbizi wa nchi hiyo na kila juhudi ya kuleta amani ya kudumu nchini humo.
Afisa huyo wa Umoja wa Mataifa ametaka juhudi zaidi zifanyike kwa ajili ya kuisaidia serikali changa ya nchi hiyo, kukabiliana na changamoto nyingi zinazoikabili.
Kouassi Lazare Etien aidha amesema, Shirika la Wakimbizi la Umoja wa Mataifa na taasisi nyingine kadhaa zisizo za kiserikali za Kiafrika zinasaidia kifedha juhudi za kurejea nyumbani wakimbizi hao na zitaendelea kufanya hivyo hadi hali itakavyorejea kuwa ya kawaida katika nchi hiyo.
Kwa mujibu wa Umoja wa Mataifa, kuna wakimbizi laki nne na 60 elfu wa Jamhuri ya Afrika ya Kati ambapo wakimbizi 11,514 kati yao wako nchi jirani.
Jamhuri ya Afrika ya Kati ilikumbwa na machafuko ya kikabila na kidini mwaka 2013 na wahanga wengi wa machafuko hayo ni raia wa kawaida hasa Waislamu.