Wananchi wa Libya waandamana kumuunga mkono Khalifa Haftar
Wananchi wa Libya wameandamana katika kona mbalimbali za nchi hiyo kutangaza uungaji mkono wao kwa Jenerali Khalifa Haftar, mkuu wa jeshi la nchi hiyo mashariki mwa nchi hiyo.
Shirika la habari la ISNA limeripoti habari hiyo na kuongeza kuwa, mamia ya wananchi wa Libya wamefanya maandamano katika miji tofauti ya nchi hiyo ili kupinga uingiliaji wa madola ya kigeni katika masuala ya ndani ya Libya. Aidha wamezitaka nchi za Marekani na za Ulaya kuondoa wanajeshi wao katika eneo la mafuta la al Hilal.
Duru moja ya kuaminika imetangaza kwamba, maandamano hayo yamefanyika sambamba na maadhimisho ya mwaka wa kukumbuka kuuawa Omar Mukhtar, shujaa wa mapambano na muqawama wa Libya.
Maandamano hayo yamefanyika katika miji ya Benghazi, Tripoli na miji mingine ya Libya kama Tobruk, al Baydhaa, Sabra, Tarhuna, Zintan, Ras al Lanuf, al Buraq na miji mingine kadhaa ya Libya, wamefanya maandamano kuliunga mkono jeshi la nchi hiyo.
Katika upande mwingine, baadhi ya duru za tiba na kijeshi za Libya zimetangaza habari ya kutokea mripuko wa bomu karibu na mahali palipofanyika maandamano hayo mjini Benghazi. Watu watano wamejeruhiwa kwenye mripuko huo.