UNHCR yataka uchunguzi ufanyike kuhusu machafuko ya Kinshasa
Umoja wa Mataifa umetaka kufanyike uchunguzi kuhusu ghasia na machafuko yaliyotokea hivi karibuni huko Kinshasa mji mkuu wa Jamhuri ya Kidemokrasia ya Kongo.
Kate Gilmore Naibu Kamishna Mkuu wa Shirika la Kuhudumia Wakimbizi la Umoja wa Mataifa UNHCR amesema akiwa mjini Geneva Uswisi kuwa kuna udharura wa kufanyika uchunguzi huru, wa wazi na wenye itibari kuhusu ghasia za hivi karibuni zilizotokea Kinshasa mji mkuu wa Jamhuri ya Kidemokrasia ya Kongo. Amesema uchunguzi huo unapasa kufanyika ili kuzuia mgogoro kati ya serikali na wapinzani wa Kongo kuwa mkubwa zaidi.
Polisi ya Kongo imedai kuwa watu wasiopungua 32 wameuawa katika ghasia za wapinzani zilizotokea Jumatatu na Jumanne wiki iliyopita, hata hivyo chama cha upinzani cha Umoja Kwa Ajili ya Demokrasia (UDPS) kimesema kuwa watu100 wameuawa katika ghasia hizo. Naibu Kamishna Mkuu wa UNHCR amesema kuwa raia 49 na polisi wanne wameuawa katika ghasia za hivi majuzi huko Kinshasa, na watu wengine 127 wamejeruhiwa. Ikiwa imesalia miezi mitatu hadi kumalizika muhula wa urais wa Rais Joseph Kabila, wapinzani huko Kongo wanasisitiza kuondoka madarakani rais huyo.