Waziri Mkuu wa Ethiopia ataka kusitishwa haraka machafuko
Waziri Mkuu wa Ethiopia ametaka kusiitishwa haraka iwezekanavyo ghasia za kisiasa nchini humo.
Hairemariam Desalegn ameeleza kuwa serikali ya Ethiopia imeazimia kuzuia kushtadi ghasia za utumiaji silaha kwa kutekeleza hali ya hatari nchini humo. Waziri Mkuu wa Ethiopia ameongeza kuwa kuendelea machafuko hayo kutaitia hatarini amani na uthabiti na kukwamisha pakubwa ustawi wa kiuchumi na kisiasa wa nchi hiyo.
Hairemariam Desalegn amesisitiza kuhusu azma ya taasisi zote za serikali ya kurejesha amani na uthabiti huko Ethiopia. Kuhusiana na suala hilo, Bi Nkosazana Dlamin Zuma Mwenyekiti wa Kamisheni ya Umoja wa Afrika pia ametilia mkazo udharura wa kurejesha amani huko Ethiopia. Taarifa ya Bi Zuma imeongeza kuwa Umoja wa Afrika unaunga mkono uamuzi wa serikali ya Ethiopia wa kutaka kutambuliwa wahusika wa tukio chungu la umwagaji damu katika mkoa wa Oromiya, ambapo raia wengi waliuliwa.
Serikali ya Ethiopia imetangaza hali ya hatari nchini humo kwa muda wa miezi sita na kutangaza siku tatu za maombolezo ya kitaifa kufuatia kuuliwa watu 52 kwenye msongamano katika hafla moja ya kidini iliyofanyika katika mji wa Bishoftu nchini humo. Msongamano huo ulijiri baada ya askari usalama wa Ethiopia kuanza kuwafyatulia risasi katika eneo walipokuwa wamekusanyika raia katika hafla hiyo ya kidini na hivyo kupata hofu na kuanza kukukimbia na kukanyagana.