Libya; njia kuu ya wahajiri wengi
https://parstoday.ir/sw/news/africa-i20044-libya_njia_kuu_ya_wahajiri_wengi
Shirika la Kimataifa la Wahajiri limetangaza kuwa Libya ni njia kuu inayotumiwa na wahajiri wengi licha ya nchi hiyo kukabiliwa na mgogoro wa ndani.
(last modified 2023-11-27T08:44:11+00:00 )
Nov 23, 2016 11:47 UTC
  • Libya; njia kuu ya wahajiri wengi

Shirika la Kimataifa la Wahajiri limetangaza kuwa Libya ni njia kuu inayotumiwa na wahajiri wengi licha ya nchi hiyo kukabiliwa na mgogoro wa ndani.

Shirika la Kimataifa la Wahajiri limesema katika ripoti yake ya wiki hii kwa mujibu wa uchunguzi mmoja wa maoni uliofanywa kwamba, asilimia 56 ya wahajiri wote ambao wako nchini Libya hawana lengo la kuelekea Ulaya bali wanapendelea kubakia katika nchi hiyo ya Kiafrika.  Shirika hilo limeongeza kuwa asilimia 81 hadi 83 ya wahajiri kutoka Misri, Chad na Sudan wanapendelea kubaki Libya huku asilimia 43 wa wahajiri wengine wakitaka kuelekea barani Ulaya.

 

Wahajiri wa Kiafrika wakiwa wamesongamana katika boti ya plastiki katika safari ya kifo ya kuelekea Ulaya

Uchunguzi huo wa maoni umefanyika baada ya kuhojiwa wahajiri 1946 katika maeneo 9 ya Libya. Pamoja na hayo yote, Shirika la Kimataifa la Wahajiri limetangaza katika ripoti yake mpya kuhusu majeruhi wa baharini huko Libya kuwa, wahamiaji 440 waliokolewa katika maji ya nchi hiyo kati ya tarehe 4 hadi 18 za mwezi huu wa Novemba.