Jeshi la Libya lasimamisha oparesheni katika eneo la Qanfuda
Msemaji wa vikosi vya ulinzi vya Libya amesema kuwa vikosi hivyo vimesimamisha operesheni ya kijeshi katika eneo la Qanfuda magharibi mwa mji wa Benghazi wa kaskazini mashariki mwa nchi hiyo ili kuwalinda raia.
Kanali Ahmed al Mismari amebainisha kuwa wamesimamisha oparesheni ya kijeshi katika eneo la Qanfuda la magharibi mwa mji wa Benghazi kwa sababu makundi yenye silaha yanazitumia kama ngao za binadamu familia za wenyeji wa eneo hilo. Kanali al Mismari ameongeza kuwa watu wanaopigana vita huko Benghazi ni raia wa nchi ajinabi na kwamba suala hilo limelipelekea jeshi la Libya kubadilisha mbinu zake za kulikomboa eneo hilo.
Libya ilitumbukia katika mgogoro mwaka 2011 baada ya kung'olewa madarakani Kanali Muammar Gaddafi, hatua iliyoibua mapigano kati ya makundi ya wanamgambo na ya kikabila nchini humo. Libya aidha imegeuka kuwa maficho ya makundi ya kigaidi kama lile la Daesh.