Khalifa Haftar apinga kufanya mazungumzo na serikali ya umoja wa kitaifa Libya
-
Jenerali Khalifa Haftar
Kamanda wa majeshi ya Libya mashariki mwa nchi hiyo amekanusha madai ya kufanyika mazungumzo ya aina yoyote kati yake na serikali huko magharibi mwa nchi hiyo katika siku zijazo.
Jenerali Khalifa Haftar Kamanda wa vikosi vya Libya vya mashariki mwa nchi hiyo amesisitiza leo kuwa, hakuna mpango wowote wa mazungumzo kati yake na Fayez al Sarraj, Waziri Mkuu wa serikali ya umoja wa kitaifa ya Libya, magharibi mwa nchi hiyo.
Khalifa Haftar ameongeza kuwa mazungumzo kati yake na Sarraj ambayo yalianza miaka miwili iliyopita yamegonga mwamba na kwamba hali ya hivi sasa nchini Libya inahitajia kuendelezwa mapambano.
Kamanda huyo wa vikosi vya Libya mashariki mwa nchi hiyo ameeleza pia kuwa, vikosi vyake hivi sasa vinashikilia karibu asilimia 80 ya ardhi ya Libya.
Shirika la habari la Reuters limenukuu duru moja iliyoko karibu na serikali ya Algeria na kuripoti kuwa, inaonekana Jenerali Haftar siku chache zijazo ataanza mazungumzo na Fayez al Sarraj huko Algeria.
Libya imegawanyika katika sehemu mbili za mashariki na magharibi baada ya kupinduliwa kiongozi wa nchi hiyo, Kanali Muammar Gaddafi mwaka 2011.