Mahakama ya Kimataifa ya Jinai (ICC) kuchunguza uhalifu waliofanyiwa wahajiri nchini Libya
Mkuu wa Mashtaka wa Mahakama ya Kimataifa ya Jinai (ICC) ametangaza kuwa mahakama hiyo imeanzisha uchunguzi kuhusu jinai na uhalifu waliofanyiwa wahajiri nchini Libya.
Fatou Bensouda, Mkuu wa Mashtaka wa Mahakama ya ICC yenye makao yake The Hague, Uholanzi amesema, kuna maelfu ya wahajiri wakiwemo wanawake na watoto katika jela za Libya na kuongeza kuwa vitendo vya ubakaji, mauaji na utesaji vimegeuka kuwa jambo la kawaida katika jela za nchi hiyo.
Huku akiashiria kuwa tangu mwaka uliopita wa 2016 hadi sasa hali ya usalama nchini Libya ni mbaya, Bensouda ametahadharisha kuhusu uhusiano uliopo baina ya wafanya magendo ya binadamu, kushamiri kwa megenge yaliyoratibiwa na kuwepo kwa mitandao ya kigaidi nchini humo.
Wafanya magendo ya binadamu wanaitumia vibaya hali ya mchafukoge ambayo imekuwa ikitawala nchini Libya tangu kuangushwa utawala wa aliyekuwa dikteta wa nchi hiyo Muammar Gadafi mwaka 2011, ambapo harakati kubwa za magendo ya binadamu wanaosafirishwa kuelekea Italia zinafanywa kutokea magharibi mwa Libya.../