Waziri Mkuu wa Congo-Brazzaville ajiuzulu, matatizo ya kiuchumi yatajwa
https://parstoday.ir/sw/news/africa-i33280-waziri_mkuu_wa_congo_brazzaville_ajiuzulu_matatizo_ya_kiuchumi_yatajwa
Waziri Mkuu wa Congo-Brazzaville ametangaza kujiuzulu wadhifa wake huo, huku mgogoro wa kiuchumi unaoikabili nchi hiyo ukitajwa kuwa sababu ya kujiuzulu kwake.
(last modified 2023-11-27T08:44:11+00:00 )
Aug 17, 2017 23:40 UTC
  • Waziri Mkuu wa Congo-Brazzaville ajiuzulu, matatizo ya kiuchumi yatajwa

Waziri Mkuu wa Congo-Brazzaville ametangaza kujiuzulu wadhifa wake huo, huku mgogoro wa kiuchumi unaoikabili nchi hiyo ukitajwa kuwa sababu ya kujiuzulu kwake.

Clément Mouamba amejiuzulu baada ya Rais Denis Sassou N'Guesso kusema kuwa, kuna haja ya kupatikana serikali mpya itakayoweza kukabiliana na matatizo ya kiuchumi ya nchi hiyo. Jumanne iliyopita, Rais Sassou N'Guesso alitangaza kuwa, nchi yake inakabiliwa na matatizo makubwa ya kiuchumi na ana wasi wasi wa kuendelea hali hiyo. Akizungumzia kuwa mgogoro wa kiuchumi uliibuka kufuatia matatizo ya kifedha na kwamba leo umekuwa suala la kijamii linaloikabili sekta ya kiuchumi, alisema kuwa hata vyanzo vya bajeti na uwekezaji vimeendelea kupungua kila uchao nchini Congo-Brazzaville.

Rais Denis Sassou N'Guesso wa Congo-Brazzaville

Hata hivyo alipongeza juhudi zilizochukuliwa katika kuzuia kufilisika kwa taifa hilo kutokana na mgogoro huo wa kiuchumi. Hii ni katika hali ambayo Shirika la Fedha la Duniani limetangaza ongezeko la deni la Congo-Brazzaville na kwamba nchi hiyo ilikuwa pia imelificha shirika hilo kuhusiana na baadhi ya madeni yake. Mbali na matatizo ya kiuchumi, serikali ya Brazzaville inakabiliwa pia na matatizo ya kisiasa ambayo yanatokana na upinzani mkubwa wa baadhi ya viongozi wa vyama vya siasa dhidi ya rais huyo, upinzani ambao umepelekea kuzaliwa kwa makundi ya waasi likiwemo kundi maarufu la Ninja ambalo limehusika na mauaji ya askari wengi wa serikali.