Taasisi ya Haki za Binadamu: Kongo inapasa kutekeleza majukumu yake kuhusu wakimbizi
Mratibu wa Kitaifa wa Taasisi Zisizo za Kiserikali katika Jamhuri ya Kidemokrasia ya Kongo ameitaka serikali ya nchi hiyo kutekeleza majukumu yake kuhusu suala la haki za wakimbizi na raia wanaotafuta hifadhi nchini humo.
William Wenga amesema kuwa wakimbizi kadhaa wa Burundi waliuawa katika mji wa Kamanyola mkoani Kivu Kusini mashariki mwa Kongo. Amesema watu 37 akiwemo mwanajeshi mmoja wa Jamhuri ya Kidemokrasia ya Kongo waliuawa katika mapigano yaliyojiri kati ya wakimbizi wa Burundi na wanajeshi wa nchi hiyo. Imebainika kuwa mauaji hayo yalitokea wakati wakimbizi wa Burundi walipokuwa wakiandamana kupinga suala la kurejeshwa nyumbani wenzao kadhaa. Wakimbizi hao walipoteza maisha baada ya kupigwa risasi na wanajeshi wa DRC.
Machafuko na ukosefu wa amani vinaendelea kushuhudiwa katika maeneo ya mashariki na kaskazini mwa Kongo kwa zaidi ya miaka ishirini sasa. Kushindwa jeshi na kikosi cha wanajeshi wa Kofia Bluu wa Umoja wa Mataifa kuwaangamiza wanamgambo kumezidisha hali ya mchafukoge mashariki mwa nchi hiyo.