Raila: Mabalozi wa nchi za Magharibi ni wasaliti, wachukuliwe hatua
https://parstoday.ir/sw/news/africa-i36297-raila_mabalozi_wa_nchi_za_magharibi_ni_wasaliti_wachukuliwe_hatua
Raila Odinga Kiongozi wa Muungano wa upinzani Kenya (Nasa) jana aliwataka viongozi wa nchi za Magharibi hususan Marekani na Uingereza kuwachukulia hatua mabalozi wanaoziwakilisha nchi hizo huko Kenya kwa kuhujumu demokrasia.
(last modified 2026-02-21T22:51:18+00:00 )
Nov 10, 2017 04:50 UTC
  • Raila: Mabalozi wa nchi za Magharibi ni wasaliti, wachukuliwe hatua

Raila Odinga Kiongozi wa Muungano wa upinzani Kenya (Nasa) jana aliwataka viongozi wa nchi za Magharibi hususan Marekani na Uingereza kuwachukulia hatua mabalozi wanaoziwakilisha nchi hizo huko Kenya kwa kuhujumu demokrasia.

Akihutubia kwenye kongamano lililoandaliwa mjini Washington, Marekani, Bw Odinga alilalamika kuwa mabalozi hao hupuuza wito wa mageuzi ya kidemokrasia mradi tu kuna utulivu na kuongeza kuwa utulivu uliopo huficha maovu mengi.

Alisema kuwa na hapa ninamnukuu: "Nimekuja kuwasilisha ujumbe mmoja: Tunahitaji vitengo vya serikali zenu vishauri mabalozi wenu nchini Kenya. Hawajafanikiwa kutatua janga lililopo na kwa hakika wamekuwa wakishirika katika kusababisha matatizo hayo,” mwisho wa kunukuu.

Raila Odinga

Kiongozi wa Muungano wa upinzani nchini Kenya (Nasa) amekosoa namna mabalozi hao walivyotilia mkazo kuwa Tume Huru ya Uchaguzi na Mipaka ya Kenya (IEBC) ilikuwa tayari kusimamia uchaguzi wa marudio kwa njia ya wazi na ya haki, licha ya Mwenyekiti wa tume hiyo, Bw Wafula Chebukati, kukariri kwamba mazingira ya uchaguzi hayakuwa sawa.

Bw Odinga alionya kuwa mgawanyiko wa kisiasa unaoshuhudiwa nchini humo usipotatuliwa kwa haraka, kuna hatari ya ukosefu wa amani na utulivu kwa njia itakayoathiri bara zima la Afrika na kwingineko duniani.

Kongamano hilo liliandaliwa na Shirika la Center for Strategic and International Studies (CSIS). Odinga alisema, njia pekee ya kurejesha hali ya kawaida nchini Kenya ni kuandaa uchaguzi mpya wa urais, kwa njia ya uwazi na itakayoaminiwa na wagombea wote.