IGAD yalaumu wanaovuruga mapatano mapya ya kusitisha vita Sudan Kusini
https://parstoday.ir/sw/news/africa-i38323-igad_yalaumu_wanaovuruga_mapatano_mapya_ya_kusitisha_vita_sudan_kusini
Mwenyekiti wa baraza la mawaziri katika Shirika la Maendeleo la Kiserikali la Nchi za Afrika Mashariki IGAD amelaani kitendo cha kuvunjika kwa makubaliano yaliyosainiwa na pande zinazohasimiana nchini Sudan Kusini.
(last modified 2023-11-27T08:44:11+00:00 )
Dec 31, 2017 00:02 UTC
  • IGAD yalaumu wanaovuruga mapatano mapya ya kusitisha vita Sudan Kusini

Mwenyekiti wa baraza la mawaziri katika Shirika la Maendeleo la Kiserikali la Nchi za Afrika Mashariki IGAD amelaani kitendo cha kuvunjika kwa makubaliano yaliyosainiwa na pande zinazohasimiana nchini Sudan Kusini.

Katika taarifa yake Workneh Gebeyehu, ameeleza masikitiko yake na kuhuzunishwa juu ya kuvurugika kwa makubaliano hayo yaliyosainiwa Alhamisi wiki iliyopita mjini Addis Ababa nchini Ethiopia.

Mwenyekiti huyo pia, amezitaka pande zinazohasimiana kuacha mara moja namna zote za mivutano, na kuwataka wahusika hao kutafakari juu ya matendo yao.

Katika taarifa yake pia, amesema kuvunjika tena kwa makubaliano mapya baada ya kusainiwa kunadhoofisha jitihada zinazofanywa na jamii ya kimataifa ambayo imeungana pamoja ili kusaidia vyama vya Sudan Kusini kutatua mgogoro kwa njia ya majadiliano jambo litakalosaidia kupatikana suluhu ya kudumu, ili kujenga taifa lao kwa njia ya kidemokrasia.

Salva Kiir na Riek Machar

Mwenyekiti huyo wa baraza la mawaziri la IGAD amesema taasisi hiyo haitaacha kuwachukulia hatua wanaovuruga makubaliano hayo kwa mujibu wa sheria ya kimataifa iliyopitishwa na wakuu wa nchi za IGAD Novemba 24 mwaka 2014

Sudan Kusini ilitumbukia katika vita vya ndani Disemba 2013 baada ya Rais Salva Kiir kutoka kabila la Dinka kumtuhumu makamu wake wa zamani, Riek Machar wa kabila la Nuer kwamba alihusika na jaribio la kuipindua serikali yake.