Gambia yawatia nguvuni majenerali wa Yahya Jammeh
Jeshi la Gambia limewatia mbaroni majenerali wawili wa ngazi za juu wa utawala wa rais wa zamani wa nchi hiyo, Yahya Jammeh.
Duru za kijeshi zimesema kuwa, Umpa Mendy na Ansumana Tamba ambao walikuwa wanaongoza Gadi ya Rais wamekamatwa baada ya kurejea nchini kutoka uhamishoni.
Wawili hao waliandamana na Jammeh alipokimbilia Equatorial Guinea baada ya kulazimika kuachia madarakani.

Itakumbukwa kuwa, baada ya kuchachamaa kwa muda na kukataa kukabidhi hatamu za uongozi wa nchi, aliyekuwa rais wa Gambia Yahya Jammeh hatimaye alikubali matokeo ya uchaguzi wa rais uliofanyika Desemba mosi mwaka 2016 na kungátuka madarakani, kufuatia mashinikizo ya kieneo na kimataifa.
Jammeh, ambaye aliitawala Gambia kwa muda wa miaka 22 aliondoka nchini humo kufuatia hali hiyo na sasa yuko uhamishoni nchini Equatorial Guinea.