Marekani yamzuia rais wa zamani wa Somalia kuingia nchini humo
Aliyekuwa rais wa Somalia amenyimwa viza ya kuingia nchini Marekani, chini ya dikrii iliyopasishwa na Rais Donald Trump ya kuzuia watu na wahajiri kutoka nchi za Kiislamu kuingia nchini humo.
Hassan Sheikh Mohamud alitazamiwa leo Jumanne kuhutubia kongamano kuhusu mgogoro wa Somalia, lenye kaulimbiu "Somalia katika Njia Panda, Fursa na Changamoto Baada ya Vita vya Wenyewe kwa Wenyewe".
Kwa mujibu wa shirika la World Council Affairs of Maine (WCM) lililoandaa kongamano hilo, rais huyo wa zamani wa Somalia amezuiwa kusafiri nchini Marekani kufuatia agizo nambari 13769 la rais, lililopiga marufuku watu kutoka nchi sita zenye idadi kubwa ya Waislamu kuingia nchini humo, kwa madai kuwa ni tishio la ugaidi kwa taifa hilo.
Rais huyo wa zamani wa Somalia alikuwa akisafiri nchini Marekani mara kwa mara katika kipindi cha uongozi wake, kati ya mwaka 2012 na 2017, na hususan alipoenda kushiriki mikutano ya Baraza Kuu la Umoja wa Mataifa mjini New York.
Somalia ni miongoni mwa nchi sita za Kiislamu zilizopigwa marufuku na Trump kusafiri Marekani, chini ya sheria mpya ya uhamiaji na kupambana na ugaidi.