Kabila afuta gwaride la maadhimisho ya uhuru DRC kutokana na uasi jeshini
Rais Joseph Kabila wa Jamhuri ya Kidemokrasia ya Kongo alifuta gwaride la jeshi katika maadhimisho ya mwaka wa 58 wa uhuru kutokana na kuwepo tetesi za uasi jeshini.
Jamhuri ya Kidemokrasia ya Congo, jana ilidhimisha kumbukumbu ya miaka 58 ya uhuru wake ilioupata kutoka kwa waliokuwa wakoloni wa taifa hilo, Ubelgiji, Juni 30 mwaka 1960.
Badala ya kushiriki katika gwaride la maadhimisho ya uhuru, Kabila alihutubia taifa kupitia televisheni inayomilikiwa na serikali Ijumaa usiku ambapo aliwahakikishia wananchi kuwa uchaguzi mkuu utafanyika kama ilivyopangwa na Tume ya Uchaguzi CENI. Vilevile ametoa wito kwa wananchi kudumisha umoja.
Kikatiba, Rais Kabila anatakiwa kuondoka ofisini Disemba wakati uchaguzi utakapofanyika lakini wafuasi wake sugu wamekuwa wakitaka aendelee kuwepo madarakani. Taarifa zinadokeza kuwa kumeibuka mgawanyiko jeshini huku baadhi ya majenerali wakidaiwa kuwa hawataki Kabila aendelee kuwepo madakrani. Kwa msingi huo, ili kuepusha kuonekana hadharani mgawanyiko wa jeshi, Kabila alumua kufutilia mbali gwaride la mwaka huu.
Duru zinasema Kabila amepoteza uungaji mkono mkubwa miongoni mwa wanajeshi na ni gadi ya rais tu inayomuunga mkono. Gadi hiyo ni sehemu ndogo sana ya jeshi la DRC. Mara ya mwisho gwaride za maadhimisho ya huru zilipoahirishwa ikuwa ni katika miaka ya 2012 na 2013 wakati nchi hiyo ilikuwa vitani na waasi wa M23.
Rais Kabila alitakikana kuondoka madarakani Disemba mwaka 2016 lakini hakufanya hivyo jambo ambalo limeibua wasiwasi wa nchi hiyo kurejea tena katika vita vya ndani ambavyo viliua mamilioni ya raia miaka ya nyuma.