IMN: Sheikh Ibrahim Zakzaky amepelekwa mahala kusikojulikana
Harakati ya Kiislamu ya Nigeria imetangaza kuwa, kiongozi wa harakati hiyo Sheikh Ibrahim Zakzaky amepelekwa mahala kusikojulikana mara baada ya kuwasili Abuja akitokea nchini India.
Ibrahim Musa, msemaji wa Harakati ya Kiislamu ya Nigeria amesema kuwa, harakati hiyo inavitaka vyombo vya usalama vinavyomshikilia Sheikh Zakzaky kuutangazia umma mahala vinapomshikilia kiongozi huyo wa Kiislamu.
Ripoti zinasema kuwa, vyombo vya usalama hata havikumruhusu Sheikh Zakzaky kuzungumza na waandishii wa habari waliomsubiria kwa masaa kadhaa katika Uwanja wa Ndege wa Abuja.
Aidha baadhi ya taarifa zinadokeza kuwa serikali ya NIgeria imempiga marufuku Sheikh Zakzaky kuondoka nje ya nchi hiyo. Kwa mujibu wa gazeti la Punch la Nigeria, baadhi ya duru zinadokeza kuwa serikali ya Nigeria imechukua uamuzi wa kumzuia Sheikh Zakzaky kuenda nje ya nchi kupata matibabu.
Alkhamisi iliyopita Sheikh Zakzaky alilazimika kuondoka New Delhi India alikokuwa amefika siku chache zilizopita kupata matibabu. Sheikh Zakzaky ameachukua uamuzi huo kutokana na kutoridhika na mchakato mzima wa matibabu pamoja na vizingiti vya usalama alivyowekewa sambamba na kunyimwa ruhusha madakatari wake anaowaamini kumtibu.
Ikumbukwe kuwa, Sheikh Ibrahim Zakzaky pamoja na mkewe walitiwa nguvuni na askari wa jeshi la Nigeria Desemba 13, 2015 katika shambulio na uvamizi uliofanywa na askari hao dhidi ya Huseiniya ya mji wa Zaria nchini humo.
Siku hiyo askari wa jeshi la Nigeria waliwafyatulia risasi watu waliokuwa wamejumuika kwenye kituo hicho cha kidini na mbele ya nyumba ya msomi huyo na kuwaua shahidi mamia miongoni mwao wakiwemo watoto wake watatu wa kiume. Sheikh Zakzaky pamoja na mke wake walijeruhiwa vibaya sana katika tukio hilo.