Watu wenye silaha Nigeria wauwa watu wasiopungua 57
Waombolezaji huko kaskazini magharibi mwa Nigeria jana waliwazika ndugu zao baada ya kuibuka mapigano kati ya kikundi cha walinda usalama wa jamii na watu wenye silaha wasiojulikana na kusababisha kuuliwa watu wasiopungua 57.
Polisi huko kaskazini magharibi mwa Nigeria imeripoti kuwa, mapigano hayo yalitokea Jumatatu wiki hii katika wilaya ya Zuru katika jimbo la Kebbi.
Imesema kuwa, watu hao wasiojulikana walikuwa wamejizatiti kwa silaha na walikuwa wakiepa oparesheni za jeshi katika jimbo jirani la Niger wakati walipokumbana na kundi hilo la ulinzi wa jamii.
Rais Muhammadu Buhari wa Nigeria amelaani mauaji hayo katika jimbi la Kebbi huku akivihimiza vikosi vya usalama kuzidisha jitihada ili kudumisha usalama wa raia.
Mwezi Januari mwaka huu serikali ya Nigeria iliyataja magenge ya uhalifu kuwa ni makundi ya kigaidi katika juhuzi za kuyawekea vikwazo vikali makundi yanayobeba silaha na majasusi wao.
Aidha mwaka jana, magenge ya uhalifu huko Nigeria yalizisambulia shule kadhaa na kuwateka nyara makumi ya wanafunzi kwa lengo la kujipatia fedha za kikomboleo kutoka kwa wananchi ili kuwaachia huru mateka.