Ugonjwa wa Surua waongezeka barani Afrika
https://parstoday.ir/sw/news/africa-i83212-ugonjwa_wa_surua_waongezeka_barani_afrika
Taarifa zinasema kumeshuhudiwa ongezeko kubwa la ugonjwa wa surua barani Afrika tokea mwanzo wa mwaka huu wa 2022.
(last modified 2023-11-27T08:44:11+00:00 )
May 03, 2022 06:21 UTC
  • Ugonjwa wa Surua waongezeka barani Afrika

Taarifa zinasema kumeshuhudiwa ongezeko kubwa la ugonjwa wa surua barani Afrika tokea mwanzo wa mwaka huu wa 2022.

Gazeti la Ufaransa la Le Monde limechapisha ripoti kuwa nchi nyingi duniani, hasa za barani Afrika, zina wasiwasi kuhusu kuongezeka magonjwa ya kuambukiza ambapo surua ni miongoni mwa magonjwa hayo.

Jumatano iliyopita Umoja wa Mataifa ulitangaza ongezeko la asilimia 80 la maambukizi ya surua  kote duniani katika miezi mitatu ya kwanza ya mwaka huu hilo likiwa ni ongezeko kubwa ikilinganishwa na muda sawa na huo mwaka jana.

Kwa mujibu wa ripoti za Shirika la Afya Duniani na Shirikia la Umoja wa Mataifa la kuhudumia Watoto UNICEF,  surua imeongezeka sana barani Afrika kutokana na ukosefu wa usawa katika kusambaza chanjo.

Mtoto akipata chanjo ya surua

Taasisi hizo mbili za Umoja wa Mataifa zimesema  janga la corona limepelekea kusitishwa mchakato wa chanzo za magonjwa mengine duniani na jambo hilo linaweza kuhatarisha maisha ya mamilioni ya watoto.

Mashirika ya Umoja wa Mataifa yanasema kumeripotiwa kesi zaidi ya 17,300 za maambukizi ya surua duniani kote katika miezi ya Februari na Machi mwaka huu. Hii ni katika hali ambayo mwaka jana katika kipindi sawa na hicho maambukizi yalikuwa 9,600

WHO inasema nchi za Afrika ndizo zinazoongoza katika maambukizi hayo mapya ya surua.

WHO inabaini kuwa surua ni ugonjwa ambao unaweza kuzuilika kwa kupokea chanjo na kwamba mabilioni ya watoto hupokea chanjo dhidi ya ugonjwa huo unaoambukiza kwa njia ya hewa. Kila mtoto anahitaji kupokea dozi mbili za chanjo dhidi ya surua, ugonjwa ambao huenea kwa kasi kubwa zaidi kuliko Ebola, homa au corona.

Hivi sasa nchi zenye idadi kubwa ya maambukizi ya surua ni pamoja na Somalia, Liberia, Yemen, Afghanistan na Ivory Coast.