Magaidi wa ADF waua wanavijiji 40 mashariki ya DRC
Raia wasiopungua 40 wameuawa katika wimbi la mashambulzi yaliyofanywa na kundi moja la kigaidi mashariki ya Jamhuri ya Kidemokrasia ya Kongo.
Kwa mujibu wa shirika la habari la Reuters, magaidi hao walivamia vijiji kadhaa baina ya Alkhamisi na juzi Jumatatu, na kuua makumi ya watu.
Duru za hospitali na asasi za kutetea haki za binadamu zinasema kuwa, watu wengi wamejeruhiwa pia katika hujuma hizo za wanamgambo wanaobeba silaha mashariki ya DRC.
Habari zaidi zinasema kuwa, magaidi wanaoshukiwa kuwa wanachama wa ADF walianza wimbi la hujuma zao kwa kuvamia vijiji vilivyoko katika mkoa wa Kivu Kaskazini.
Inaarifiwa kuwa, wanamgambo hao waliwashambulia wanavijiji hao kwa madai kuwa wametokea katika mkoa jirani wa Ituri, na kuingia Kivu Kaskazini kutafuta maji na ardhi ya kulisha mifugo yao karibu na Mto Ituri.
Mathe Mupanda Solomon, muuguzi katika hospitali moja katika eneo hilo amesema binafsi ameshuhudia maiti 26, na kuongeza kwamba wanavijiji wengine zaidi ya 70 wametekwa nyara na magaidi hao.
Zaidi ya makundi ya wanamgambo 120 yamesambaa mashariki mwa Jamhuri ya Kidemokrasia ya Congo, na kuna mashambulizi ya mara kwa mara dhidi ya raia katika maeneo hayo.