Apr 15, 2024 13:46 UTC
  • Amir Abdollahian: Israel ikiendeleza chochoko itapewa kichapo kikubwa zaidi

Waziri wa Mambo ya Nje wa Iran amekosoa uungaji mkono wa Ujerumani kwa utawala wa Kizayuni wa Israel na kusema kuwa, iwapo utawala wa Israel unataka kuendelea na chokochoko zake, majibu yake yatakuwa ya haraka na makubwa zaidi.

Waziri wa Mambo ya Nje wa Iran Hossein Amir Abdollahian ameyasema hayo katika mazungumzo yake ya pili ya simu na Waziri wa Mambo ya Nje wa Ujerumani, Annalena Baerbock, na kueleza kuwa lengo la Jamhuri ya Kiislamu ya Iran ni kuuonya utawala wa Israel ili uelewe madhara ya kuvuka mistari nyekundu. 

Amir Abdollahian amefafanua oparesheni madhubuti ya jeshi la Iran dhidi ya utawala wa Kizayuni wa Israel na kusema kuwa, Jamhuri ya Kiislamu ilifanya oparesheni ndogo na makini dhidi ya vituo vya kijeshi vya utawala huo ghasibu, vilivyotumiwa kushambulia ubalozi mdogo wa Iran mjini Damascus.

Amir Abdollahian

Waziri wa Mashauri ya Kigeni wa Iran ameeleza matumaini yake kuwa badala ya kulaani hatua hiyo halali ya Iran, juhudi za Ujerumani zielekezwe katika kusimamisha vita katika Ukanda wa Gaza na kuimarisha amani na usalama endelevu kuanzia Bahari ya Mediterania hadi Bahari Nyekundu.

Kwa upande wake, Waziri wa Mashauri ya Kigeni wa Ujerumani amesisitiza umuhimu wa kuanza mazungumzo katika kipindi hiki hatari na kusema kuwa, matukio ya sasa yamezidisha hali ya taharuki katika eneo Magharibi mwa Asia na yamaonesha kuwa hali ya wasiwasi inaongezeka.