Pezeshkian: Iran itaendelea kuunga mkono Muqawama wa Palestina
https://parstoday.ir/sw/news/iran-i115982-pezeshkian_iran_itaendelea_kuunga_mkono_muqawama_wa_palestina
Rais wa Iran, Masoud Pezeshkian amesema kuwa, serikali yake iko tayari kutoa uungaji mkono usiotetereka kwa ajili ya mapambano ya mataifa yote yanayodhulumiwa duniani kote, hususan Muqawama wa Palestina dhidi ya utawala ghasibu wa Israel.
(last modified 2024-09-03T23:34:04+00:00 )
Sep 03, 2024 23:34 UTC
  • Pezeshkian: Iran itaendelea kuunga mkono Muqawama wa Palestina

Rais wa Iran, Masoud Pezeshkian amesema kuwa, serikali yake iko tayari kutoa uungaji mkono usiotetereka kwa ajili ya mapambano ya mataifa yote yanayodhulumiwa duniani kote, hususan Muqawama wa Palestina dhidi ya utawala ghasibu wa Israel.

Rais Pezeshkian aliyasema hayo katika ujumbe 'mzito' uliotolewa wakati wa duru ya tisa ya Mkutano wa Kimataifa wa Mujahidina Walioko Uhamishoni, uliofanyika katika Chuo Kikuu cha Damghan katika mkoa wa Semnan, kaskazini mwa Iran jana Jumanne.

Dakta Pezeshkian amebainisha kuwa, "Tangu mwanzo wa uongozi wangu serikalini, nimetangaza uungaji mkono wangu thabiti kwa watu wa Palestina na wanaokandamizwa kote ulimwenguni, nikionyesha dhamira yangu ya kutetea haki zao katika medani zote." 

Pezeshkian ameashiria urithi wa karibu nusu karne wa Jamhuri ya Kiislamu ya Iran, ambayo imekuwa ikitetea na kupigani haki, uadilifu na haki za binadamu duniani kote.

Makundi ya Muqawama katika eneo

Rais wa Iran ametoa hakikisho kwamba, chini ya uongozi wa Kiongozi Muadhamu wa Mapinduzi ya Kiislamu, Ayatullah Sayyid Ali Khamenei, juhudi hizo za kupigania haki na uadilifu duniani zitatekelezwa kwa nguvu na hekima na utawala wake, kama zilivyofanya serikali zilizopita.

Kadhalika Dakta Pezeshkian amemuenzi marehemu Waziri wa Mambo ya Nje wa Iran, Hossein Amir-Abdollahian kama mwanadiplomasia mashuhuri na mfano halisi wa diplomasia ya Muqawama.

Amir-Abdollahian alifariki dunia katika ajali ya helikopta mwezi Mei mwaka huu, pamoja na Rais wa wakati huo, Ebrahim Raisi na maafisa wengine.