Iran na Russia zajadili masuala ya kieneo na kimataifa
Waziri wa Mambo ya Nje wa Jamhuri ya Kiislamu na Iran na mwenzake wa Russia wamefanya mazungumzo kwa njia ya simu na kujadiliana kuhusiana na matukio ya kieneo na kimataifa.
Muhammad Javad Zarif na Sergei Lavrov wamejadiliana juu ya matukio ya hivi sasa katika eneo hili la Mashariki hususan mgogoro wa kisiasa na machafuko yanayoendelea nchini Syria. Wawili hao wamesisitiza juu ya umuhimu wa kuanzishwa mikakati ya pamoja ya kulisaidia taifa la Syria ambalo limeshuhudia machafuko na harakati za kigaidi kwa zaidi ya miaka mitano sasa.
Aidha katika mazungumzo hayo ya simu, Muhammad Javad Zarif, Waziri wa Mambo ya Nje wa Iran na mwenzake wa Russia Sergei Lavrov wamejadiliana juu ya kuimarisha uhusiano wa pande mbili katika nyuga tofauti.
Haya yanajiri siku chache baada ya Marais Hassan Rouhani wa Jamhuri ya Kiislamu ya Iran na Vladimir Putin wa Russia waliokwenda Azerbaijan kushiriki mkutano wa pande tatu, kukutana pambizoni mwa mkutano huo ambapo mbali na kuzungumzia masuala ya pamoja ya Moscow na Tehran walibadilishana mawazo pia kuhusiana na masuala mbalimbali yanayojiri hivi sasa ulimwenguni.
Suala la kuimarishwa uhusiano wa pande mbili ni jambo lililopewa kipaumbele katika mazungumzo ya Marais wa Jamhuri ya Kiislamu ya Iran na Russia huko mjini Baku Azerbaijan.