Iran: Jeshi liko tayari kukabiliana na chokochoko zozote za maadui
Kamanda Mkuu wa jeshi la Jamhuri ya Kiislamu ya Iran, Meja Jenerali Ataollah Salehi amesema jeshi limejiweka tayari kukabiliana na chokochoko zozote zile za maadui.
Katika ujumbe aliotoa kwa mnasaba wa Siku ya Jeshi ya kuenzi hamasa iliyotekelezwa na vikosi vya nchi kavu inayoadhimishwa rasmi hapo kesho, Meja Jenerali Salehi amesema: "Leo jeshi la Jamhuri ya Kiislamu liko katika awamu mpya ya kuleta amani na fahari kwa kujikita katika maeneo ya kijiografia ya nje ya mipaka ya Jamhuri ya Kiislamu na kwenye maji ya mbali licha ya vitisho vya nje ya eneo ili kudhamini maslahi ya taifa. Aidha kwa ushirikiano na vikosi vyengine vya ulinzi na kwa kutegemea imani na uwezo usio na ukomo wa Mwenyezi Mungu limeonyesha nguvu na uwezo mpya lilionao kwa ajili ya kukabiliana kikamilifu na chokochoko zozote za wanaoitakia mabaya Iran ya Kiislamu".
Katika miaka ya karibuni, Iran imepiga hatua kubwa katika sekta ya ulinzi na kujitegemea katika uundaji na uzalishaji zana za kijeshi.
Wakati huohuo kamanda wa jeshi la wanamaji la Jamhuri ya Kiislamu ya Iran Adimeri Habibollah Sayyari amesema licha ya kuvurugika amani na usalama katika eneo la Mashariki ya Kati Iran ina amani na usalama thabiti ambao ni matunda ya kuwa na vikosi vya ulinzi imara na vyenye utayarifu.
Akihutubia wafanyakazi wa eneo la pili la bahari ya Jasak kusini mwa nchi, Adimeri Sayyari amesema, chanzo cha machafuko na ukosefu wote wa amani unaoshuhudiwa katika eneo ni uwepo haramu wa Uistikbari wa dunia.../