Iran yakanusha madai ya Trump ya kuipatia Yemen makombora
Kamanda wa Jeshi la Walinzi wa Mapinduzi ya Kiislamu amekanusha madai yasiyo na msingi ya Rais wa Marekani kuwa eti Yemen imepokea makombora kutoka Jamhuri ya Kiislamu ya Iran.
Rais Donald Trump wa Marekani siku ya Jumapili alitoa madai yasiyo na msingi na kusema Iran inabeba jukumu la shambulizi la kombora la Jeshi la Yemen lililolenga uwanja wa kimataifa wa ndege mjini Riyadh, Saudi Arabia.
Kamanda wa Jeshi la Walinzi wa Mapinduzi ya Kiislamu, IRGC, Meja Jenerali Mohammad Ali Jaafari akizungumza na waandishi habeari ameashiria madai hayo ya Trump na kusema, "matamshi yasiyo na msingi ya Trump ni kati ya tuhuma nyingi dhidi ya Iran."
Kamanda wa IRGC ameongeza kuwa, Iran haina uwezo wa kufikishia Yemen makombora na kwamba: "Makombora ya Yemen yenye uwezo wa kulenga shabaha masafa marefu zaidii kuliko huko nyuma ni ya nchi hiyo."
Jana usiku kikosi cha makombora cha jeshi la Yemen na vikosi vya kujitolea vya wananchi kilifyatua kombora la balistiki la masafa marefu aina ya Borkan H2 na kuulenga uwanja wa ndege wa kimataifa wa Mfalme Khalid ulioko kwenye mji mkuu wa Saudi Arabia, Riyadh.
Aidha Meja Jenerali Jaafari ameashiria matamshi ya Saad Hariri aliyejiuzulu jana kama Waziri Mkuu wa Lebanon ambapo alitoa tuhuma kuwa eti Iran inaingilia masuala ya eneo. Kamanda Jaafari amesema Hariri amejiuzulu kufuatia agizo la utawala wa Kizayuni na Saudi Arabia.
Jana Hariri alitangaza kujiuzulu wadhifa wake huo katika hotuba aliyotoa akiwa nchini Saudi Arabia huku akitoa madai kuwa eti Iran inaingilia amsuala ya ndani ya nchi za Kiarabu ikiwemo Lebanon na kwamba eti harakati ya Hizbullah ya Lebanon inatekeleza matakwa ya Iran katika eneo.