Qassemi: Iran inasaidia juhudi za kuimarisha amani Mashariki ya Kati
Msemaji wa Wizara ya Mambo ya Nje ya Iran amesema kuwa sera na siasa zisizobadilika za Jamhuri ya Kiislamu ya Iran ni kusaidia jitihada za kuimarisha amani na utulivu katika eneo la Mashariki ya Kati.
Bahram Qassemi ambaye alikuwa akijibu matamshi yaliyotolewa na Mfalme wa Jordan kuhusu siasa za kieneo za Iran amesema matamshi hayo yanapingana na uhakika wa mambo, matakwa ya wananchi na nchi nyingi za eneo la Mashariki ya Kati.
Qassemi ameashiria madai kama yale ya "hilali ya Kiirani" na eti "uingiliaji" wa Iran katika masuala ya ndani ya nchi za eneo hili na kusema: Matamshi kama haya yasiyo ya kiadilifu hayawezi kuficha na kukana mchango mkubwa wa Jamhuri ya Kiislamu katika kuimarisha amani na kupambana na ugaidi.
Msemaji wa Wizara ya Mambo ya Nje ya Iran ameongeza kuwa, matamshi hayo ya Mfalme wa Jordan ambayo ni kinyume kabisa na ukweli wa mambo ambayo yametolewa katika kipindi nyeti cha sasa hayawezi kudhamini maslahi ya nchi na watu wa Mashariki ya Kati na zaidi yanahudumia malengo na maslahi ya wavamizi wasiostahamili kuona ustawi wa kiuchumi, amani na kujitawala kwa mataifa ya eneo hili.