Velayati: Iran ni nchi muhimu katika eneo la Asia Magharibi
Mshauri wa Kiongozi Muadhamu wa Mapinduzi ya Kiislamu katika Masuala ya Kimataifa amesema kuwa Iran ni nchi muhimu katika eneo la Asia ya Magharibi na inayo haki ya kujibu na kuitikia miito ya nchi rafiki na mhimili wa muqawama.
Dakta Ali Akbar Velayati ameongeza kuwa washauri wa kijeshi wa Iran wapo Iraq na Syria kufuatia maombi ya serikali halali za nchi hizo na wako huko pia kwa ajili ya kuwasaidia wananchi madhlumu wa nchi hizo na si kwa lengo jingine lolote.
Mshauri wa Kiongozi Muadhamu wa Mapinduzi ya Kiislamu Katika Masuala ya Kimataifa aliyasema hayo jana Jumatatu hapa Tehran mbele ya waandishi wa habari pambizoni mwa kikao cha baraza la ushauri cha Mkutano wa Kimataifa wa Ahlul-Bait (A.S). Dakta Velayati amebainisha kuwa Iran itaendeleza siasa zake za kushiriki vilivyo kirafiki katika eneo hili na kwamba nchi za Magharibi zipo katika eneo la Mashariki ya Kati kinyume na sheria za kimataifa tofauti na Iran.
Kuhusu kutunguliwa ndege ya kivita ya utawala chokozi wa Kizayuni, Dakta Ali Akbar Velayati ameeleza kuwa: Syria ikiwa moja ya nchi muhimu zilizo mstari wa mbele katika muqawama ina haki ya kuilinda ardhi yake nzima na kutoa jibu kwa uchokozi unaofanywa na ndege vamizi za Israel.