Mawaziri wa Mashauri ya Kigeni ya Iran na Russia wajadili masuala mbalimbali
Mawaziri wa Mashauri ya Kigeni ya Jamhuri ya Kiislamu ya Iran na Russia wamefanya mazungumzo kwa njia ya simu na kujadili masuala mbalimbali ya uhusiano wa pande mbili, ya kieneo na kimataifa.
Katika mazungumzo yao hayo kwa njia ya simu, Dakta Muhammad Javad Zarif, Waziri wa Mashauri ya Kigeni ya Jamhuri yya Kiislamu ya Iran na Sergei Lavrov, Waziri wa Mashauri yya Kigeni ya Russia wamezungumzia masuala kadhaa ikiwemo hatua ya hivi karibuni ya Russia ya kupigia kura ya veto muswada dhidi ya Iran uliowasilishwa na Uingereza katika Baraza la Usalama la Umoja wa Mataifa.
Itakumbukwa kuwa, Jumatatu iliyopita Baraza la Usalama la Umoja wa Mataifa liliitisha kikao kwa ajili ya kujadili miswada miwili kuhusiana na Yemen.
Muswada wa kwanza uliokuwa umependekezwa na Iran ulikuwa ukiituhumu Iran kwamba, inapeleka silaha huko nchini Yemen. Muswada huo uligonga ukuta na kutopasishwa baada ya Russia kuupigia kura ya veto.
Aidha muswada wa pili uliokuwa umewasilishwa na Russia na uliokuwa ukitaka kuongezwa muda mwingine wa mwaka mmoja vikwazo vya silaha dhidi ya Yemen ulipasishwa na wanachama wote wa Baraza la Usalama la Umoja wa Mataifa.
Wachambuzi wengi wa mambo wamesema kuwa, kutopasishwa muswada uliokuwa umependekezwa na Uingereza na kuungwa mkono na Marekani na Ufaransa na ambao uliokuwa dhidi ya Jamhuri ya Kiislamu ya Iran ni pigo kubwa kwa Marekani na washirika wake.