Iran yajibu ripoti ya uongo ya nchi nne za Kiarabu dhidi yake
Msemaji wa Wizara ya Mambo ya Nje ya Iran, Bahram Qassemi amekosoa ripoti ya pamoja ya nchi nne za Kiarabu iliyotolewa mbele ya Katibu Mkuu wa Jumuiya ya Nchi za Kiarabu, Ahmed Aboul-Gheit na kusema ni ya uongo na isiyo na ithibati yoyote.
Usiku uliopita Mawaziri wa Mambo ya Nje wa Jumuiya ya Nchi za Kiarabu (Arab League) walikutana mjini Riyadh, Saudi Arabia na kutoa taarifa ya pamoja wakidai kwamba eti Jamhuri ya Kiislamu ya Iran inaingilia masuala ya ndani ya nchi za Kiarabu na kwamba eti hatua hiyo imekuwa ikitishia usalama wa eneo hili. Kadhalika mawaziri hao walirejea madai ya mara kwa mara ya Umoja wa Falme za Kiarabu (Imarati) inayodai kuwa inamiliki visiwa vitatu vya Iran vya Abu Musa, Tomb Kubwa na Tomb Ndogo huku wakitangaza kuiunga mkono Abu Dhabi kwa hatua yoyote ile katika uwanja huo.
Bahram Qassemi, Msemaji wa Wizara ya Mambo ya Nje ya Iran amesema kuwa, tuhuma hizo bandia dhidi ya Iran ya Kiislamu ni za kipuuzi na kwamba zinatokana na kuchanganyikiwa viongozi wa nchi hizo za Kiarabu. Amesema, kuendelea mwenendo huo wa kiuhama dhidi ya taifa la Iran, kutazidi kuliepusha eneo la Mashariki ya Kati na amani na utulivu. Kadhalika Qassemi sambamba na kuashiria mienendo ya uhasama na haribifu ya baadhi ya nchi za Kiarabu katika kupotosha fikra za walio wengi kuhusiana na matukio ya eneo la Mashariki ya Kati, ameonyesha kusikitishwa na misimamo hiyo ya kiuadui ya madola ya Kiarabu dhidi ya taifa hili badala ya kumtambua adui halisi wa umma wa Kiislamu yaani utawala haramu wa Israel.
Hata hivyo Msemaji wa Mambo ya Nje ya Iran amesema ana matumaini kwamba katika vikao vinavyoendelea vya Arab League mjini Riyadh, viongozi wa nchi za Kiarabu wataweza kubaini kiini halisi cha migogoro katika eneo la Mashariki ya Kati badala ya kuendelea kutoa tuhuma zisizo na maana dhidi ya Iran ya Kiislamu.