IMF: Iran ikabiliane na vikwazo vya kiuchumi vya Marekani
Mfuko wa Fedha wa Kimataifa (IMF) umeiagiza Iran kuimarisha zaidi uchumi wake ili kukabiliana na vikwazo vya Marekani.
Gerry Rice msemaji wa IMF amesema kuwa, Iran inapaswa kuimarisha sera za kulinda uchumi wake katika kukabiliana vikwazo vipya vya Marekani ambavyo vinaweza kuathiri ustawi wa kiuchumi na uuzaji nje wa mafuta ya nchi hiyo.
Rais Donald Trump wa Marekani tarehe 8 Mei alichukua hatua na uamuzi wa upande mmoja wa kuiondoa nchi hiyo katika makubaliano ya nyuklia ya JCPOA na wakati huo huo atakangaza kuirejeshea Iran vikwazo vya nyuklia na washirika wa kibiashara wa Tehran.
Uingereza, Ufaransa, Russia, Uchina, Ujerumani na Umoja wa Ulaya zimetangaza kuunga mkono makubaliano hayo ya nyuklia na kupendekeza mfumo maalumu wa utendaji kwa ajili ya kuendeleza biashara na Iran katika kipindi hiki cha vikwazo vya Marekani.
Nchi na wanunuzi wakubwa wa mafuta ya Iran kama China na India zimepinga matakwa ya Marekani dhidi ya Iran na kusisitiza kuwa zitaendelea kufanya biashara na jamhuri ya Kiislamu. Vilevile nchi wanachama katika makubaliano ya nyuklia ya JCPOA zimepinga hatua ya uhasama ya Rais Donald Trump wa Marekani na kuyataka makampuni ya nchi hizo kudumisha biashara na Jamhuri ya Kiislamu ya Iran.