Amir Hatami: Iran inatoa uungaji mkono wa kimaanawi kwa mataifa madhulumu
Waziri wa Ulinzi wa Jamhuri ya Kiislamu ya Iran amesema kuwa, taifa hili linatoa uungaji mkono wa kimaanawi kwa uwezo wake wote kwa mataifa madhlumu ulimwenguni.
Brigedia Jenerali Amir Hatami amesema kuwa, muqawama na mapambano ya wananchi huko Lebanon, Palestina, Iraq na Syria yameimarika na kukita mizizi na kuongeza kuwa, Wamarekani walianzisha makundi ya kigaidi na kutwaa kwa mabavu sehemu kubwa ya ardhi ya Iraq na Syria lakini fikra ya muqawama na mapambano ndiyo iliyotoa pigo na kuwashinda na hatimaye kukomboa maeneo hayo.
Waziri wa Ulinzi wa Jamhuri ya Kiislamu ya Iran ameashiria mapambano na muqawama wa wananchi wa Yemen dhidi ya Saudi Arabi na washirika wake na kusema kuwa, utawala wa Aal Saud ulianzisha muungano na kupata baraka za Marekani sambamba na kununua silaha nyingi na kuishambulia Yemen na wahusika walikuwa wakidhani kwamba, wataishinda nchi hiyo, lakini wanamapambano wa Yemen wamekabiliana na wavamizi hao wakiwa mikono mitupu.
Waziri wa Ulinzi wa Iran amesema kuwa, hii leo mambo yamewawia vigumu Wamarekani kiasi kwamba, sasa Washington inachokifikiria ni kutoa tuhuma za uongo na zisizo na msingi wowote dhidi ya Iran.
Brigedia Jenerali Amir Hatami ameashiria vikwazo vya Marekani dhidi ya Iran na kusema kuwa, kama ambavyo taifa hili liliweza kubadilisha vita vya kutwishwa vilivyoanzishwa na dikteta wa zamani wa Iraq, Saddam na kuvifanya kuwa fursa ya kujiimarisha na kupata nguvu zaidi kiulinzi, vivyo hivyo, vikwazo hivi vinatumiwa ili kuondoa mapungufu ya kiuchumi ya taifa hili.