Iran: Uingiliaji wa US, NATO umeshadidisha mgogoro wa Ukraine
Jamhuri ya Kiislamu ya Iran imekosoa vikali chokochoko za Marekani na shirika la kijeshi la NATO katika mgogoro wa Ukraine na kusisitiza kuwa, uingiliaji huo umeshadidisha taharuki mashariki mwa nchi hiyo jirani na Russia.
Saeed Khatibzadeh, Msemaji wa Wizara ya Mashauri ya Kigeni ya Jamhuri ya Kiislamu ya Iran amesema pande zote husika kwenye mgogoro huo zinapaswa kujizuia kuchukua hatua yoyote inayoweza kushadidisha hali ya mambo.
Khatibzadeh alisema hayo jana Jumanne katika taarifa na kuongeza kuwa, "kwa bahati mbaya, uingiliaji wa mambo, na hatua za uchochezi za NATO ikiongozwa na Marekani zimefanya hali ya mambo kuwa mbaya zaidi katika eneo hilo."
Msemaji wa Wizara ya Mashauri ya Kigeni ya Jamhuri ya Kiislamu ya Iran ameongeza kuwa, Tehran inafuatilia masuala yanayofungamana na mgogoro wa Ukraine kwa mazingatio makubwa.
Jumatatu usiku, muda mfupi baada ya Russia kutambua rasmi uhuru wa maeneo ya Luhansk na Donetsk nchini Ukraine, Baraza la Usalama liliitisha kikao cha dharua kujadili suala hilo.
Eneo la Donbass lililo mashariki mwa Ukraine linaundwa na mikoa ya Donetsk na Luhansk, pamoja na maeneo mengine kadhaa yenye wakazi wenye asili ya Russia, na majimbo hayo mawili yalijitangazia uhuru na kujitenga na Kiev mwaka 2014 baada ya mabadiliko ya serikali nchini Ukraine.