UN: Israel imebomoa majengo 54 ya Wapalestina mwezi Julai
https://parstoday.ir/sw/news/west_asia-i100468-un_israel_imebomoa_majengo_54_ya_wapalestina_mwezi_julai
Ripoti ya Umoja wa Mataifa imebaini kuwa vikosi vya kijeshi vya utawala haramu wa Israel vilibomoa majengo 54 yanayomilikiwa na Wapalestina huko Al-Quds (Jerusalem) Mashariki katika tarafa kubwa zaidi ya eneo la Ukingo wa Magharibi linalokaliwa kwa mabavu mwezi Julai.
(last modified 2023-11-27T08:44:11+00:00 )
Jul 30, 2023 01:07 UTC
  • UN: Israel imebomoa majengo 54 ya Wapalestina mwezi Julai

Ripoti ya Umoja wa Mataifa imebaini kuwa vikosi vya kijeshi vya utawala haramu wa Israel vilibomoa majengo 54 yanayomilikiwa na Wapalestina huko Al-Quds (Jerusalem) Mashariki katika tarafa kubwa zaidi ya eneo la Ukingo wa Magharibi linalokaliwa kwa mabavu mwezi Julai.

Kwa mujibu wa Ofisi ya Umoja wa Mataifa ya Kuratibu Masuala ya Kibinadamu (OCHA), jumla ya Wapalestina 66, wakiwemo watoto 34, walikimbia makazi yao kutokana na bomoabomoa iliyotokea kati ya Julai 5 na 24,  ambapo Wapalestina wengine zaidi ya 795 waliathirika kimaisha.

Chombo hicho cha Umoja wa Mataifa kimesema katika ripoti yake kwamba majengo 16 kati ya yaliyobomolewa yalijengwa kwa fedha za  wafadhili.

Ripoti hiyo imeonyesha kuwa asilimia 80 ya miundo iliyoathiriwa (43) ilikuwa katika eneo C la Ukingo wa Magharibi, ambalo linajumuisha asilimia 61 ya eneo hilo na liko chini ya udhibiti kamili wa kijeshi wa Israeli.

Zaidi ya hayo, utawala haramu wa Israel ulibomoa majengo mawili yanayohusiana na kilimo katika wilaya ya Birin ya Ukingo wa Magharibi kwa kisingizio cha uwongo cha kuingilia ardhi inayomilikiwa na utawala huo.

Buldoza ya utawala wa Kizayuni ikibomoa maeneo ya Wapalestina

Ripoti ya OCHA imesema wanajeshi wa Israel, pamoja na kubomoa na kuwafukuza watu kwa nguvu, waliwapiga risasi na kuwaua Wapalestina 10, miongoni mwao wakiwemo watoto, kati ya Julai 4 na 27 wakati wa mashambulizi tofauti huko Nablus, Qalqilya na Ramallah.

Zaidi ya hayo, shirika hilo la Umoja wa Mataifa lilisema, Wapalestina 352, ikiwa ni pamoja na watoto 56, walijeruhiwa na majeshi ya Israeli katika Ukingo wa Magharibi katika kipindi kilichotajwa. Kwa uchache watoto 26 walipigwa risasi za moto.

Israel mara kwa mara hubomoa nyumba za Wapalestina katika Ukingo wa Magharibi wa Mto Jordan na Quds Mashariki inayokaliwa kwa mabavu, kwa madai kuwa majengo hayo yamejengwa bila vibali, jambo ambalo ni vigumu kukubalika. Pia wakati mwingine huwaamuru Wapalestina kubomoa nyumba zao wenyewe au kulipa gharama za ubomoaji.