Waziri wa Ulinzi: Jeshi la Syria bado liko Hama
-
Luteni Jenerali Abbas
Waziri wa Ulinzi wa Syria, Luteni Jenerali Ali Mahmoud Abbas, amesema kuwa hali ya mambo katika mji wa Hama imedhibitiwa na kwamba kusonga mbele kwa awali magaidi wa Kitakfiri katika mji huo kulitokana na mbinu za muda za vikosi vya ulinzi vya nchi hiyo
Luteni Jenerali Abbas ametoa hakikisho kuwa vikosi vya ulinzi vya Syria bado vipo katika viunga vya mji wa Hama na vimejiandaa kikamilifu kutekeleza majukumu yao ya kitaifa na kikatiba.
Waziri wa Ulinzi wa Syria ameahidi kuwa jeshi la nchi hiyo halitosita kurejesha amani na utulivu katika maeneo yaliyovamiwa na magaidi.
"Jeshi la Syria litasalia kuwa bwawa lisiloweza kuvukwa mbele ya yeyote anayetaka kuhujumu usalama wa Syria," amesema Luteni Jenerali Ali Mahmoud Abbas.
Waziri wa Ulinzi wa Syria ameyalaani makundi ya Kitafkiri akiyataja kuwa taasisi za kigaidi za kikatili zaidi zinazoungwa mkono na nchi za kanda hii na nyingine ajinabi. Amesema, nchi hizo zinawapa magaidi hao misaada ya kijeshi na kilojistiki ili kufanya hujuma dhidi ya Syria.
Jeshi la Syria limeahidi kuendeleza oparesheni zake ili kuzima mashambulizi ya makundi hayo yanayosaidiwa na nchi za kigeni katika maeneo ya kaskazini magharibi mwa nchi hiyo.