Kwa nini Iran inakaribisha upanuzi wa ushirikiano na Afghanistan?
https://parstoday.ir/sw/news/west_asia-i123542-kwa_nini_iran_inakaribisha_upanuzi_wa_ushirikiano_na_afghanistan
Majadiliano na mikutano ya maafisa wa Iran na Afghanistan yanaendelea kwa lengo la kupanua uhusiano na kutatua masuala kati ya nchi hizi mbili.
(last modified 2025-03-05T22:56:01+00:00 )
Mar 05, 2025 22:56 UTC
  • Kwa nini Iran inakaribisha upanuzi wa ushirikiano na Afghanistan?

Majadiliano na mikutano ya maafisa wa Iran na Afghanistan yanaendelea kwa lengo la kupanua uhusiano na kutatua masuala kati ya nchi hizi mbili.

"Ali Akbar Pourjamshidian", Naibu Waziri wa Mambo ya Ndani wa Iran, alipokutana karibuni na ujumbe wa Afghanistan jijini Tehran, alisisitiza juu ya ushirikiano zaidi katika mapambano dhidi ya dawa za kulevya na kusema: "Kuzuia upandaji, ununuzi na uuzaji wa dawa za kulevya nchini Afghanistan ni hatua nzuri sana ambayo, kwa mkakati wa pamoja wa serikali ya Afghanistan, inaweza kuleta matokeo mazuri zaidi."

Naibu Waziri wa Mambo ya Ndani alibainisha kuwa kuna takriban wakimbizi wa Afghanistan milioni 4.5 walioko kihalali nchini Iran, pamoja na wengine milioni 2 walioko nchini kinyume cha sheria. Amesema kuwa dhamira ya taifa na serikali ya Iran ni kushirikiana zaidi na watu na serikali ya Afghanistan ili kutatua matatizo yaliyopo.

Mullah Abdulhaq Hamkar, Naibu Waziri wa Mambo ya Ndani wa Afghanistan anayeshughulikia mapambano dhidi ya dawa za kulevya, pia ameshukuru Iran kwa kuwapokea Wakimbizi wa Afghanistan kwa miongo kadhaa iliyopita na kusema: "Familia zetu zimeishi kwa amani nchini Iran kwa miaka mingi."

Katika miezi ya hivi karibuni, majadiliano ya mara kwa mara kati ya maafisa wa Tehran na Kabul yameendelea kwa lengo la kupanua uhusiano katika nyanja mbalimbali za uchumi, siasa, na utamaduni pamoja na kutatua masuala kama vile mapambano dhidi ya dawa za kulevya, usalama wa mipaka, kupambana na uhamiaji haramu wa Waafghanistan kuja Iran, na haki za maji.

Safari ya hivi karibuni ya "Seyed Abbas Araghchi", Waziri wa Mambo ya Nje wa Iran, jijini Kabul ilifanyika kwa madhumuni ya kufuatilia haki ya Iran kutoka kwa jirani yake huyo wa mashariki. Viongozi wa Afghanistan pia wamekubali kushirikiana ili kutimiza matakwa ya Iran na kupanua ushirikiano wa pande mbili. Bila shaka, kuongezeka kwa ushirikiano kati ya Iran na Afghanistan kutakuwa na athari chanya kwa uchumi, usalama na utulivu wa nchi hizi mbili pamoja na eneo zima.

Jamhuri ya Kiislamu ya Iran, iwe sasa au katika miaka ya nyuma, daima imekuwa ikishirikiana kwa nia njema na watawala wa Afghanistan. Ni wazi kuwa kuendelea kwa uhusiano huu kunategemea kutimizwa kwa ahadi zilizotolewa na maafisa wa Afghanistan.

                      Seyed Abbas Araghchi  (kushoto) na Mullah Abdulhaq Hamkar 
 

 Ukarimu wa Iran kwa zaidi ya miaka 40 kwa wakimbizi wa Afghanistan unaonyesha mshikamano wa kina kati ya watu wa mataifa haya mawili na umuhimu wa uhusiano wa kirafiki kati ya Iran na Afghanistan. Iran imetoa elimu ya bure, huduma za afya, na fursa za kijamii kwa wakimbizi wa Afghanistan, hasa wakati wa mlipuko wa ugonjwa wa COVID-19.

Mbali na kuwakaribisha wakimbizi, Iran pia ina sera za wazi na madhubuti kuhusu utulivu wa kisiasa na usalama wa Afghanistan. Nchi hiyo ina fursa kubwa za uwekezaji, na Iran imekuwa mstari wa mbele katika kuwekeza na kujenga upya miundombinu ya uchumi, viwanda, na uzalishaji wa Afghanistan, hasa katika sekta ya kilimo.

Katika miaka ya hivi karibuni, Iran imeunda njia za reli, barabara na usafiri wa baharini ili kuwezesha biashara ya Afghanistan kufikia masoko ya kimataifa.

Reli ya "Khaf-Herat" na bandari ya Chabahar, iliyoko kusini mashariki mwa Iran, ni mifano ya juhudi hizo.

Serikali ya 14 ya Iran inafanya kazi ili kukamilisha reli yake upande wa mashariki mwa nchi na kuiunganisha na reli kuu ya Iran, ambayo itaiwezesha Afghanistan kufikia bahari. Kwa njia hii, wafanyabiashara wa Afghanistan wataweza kusafirisha bidhaa zao kupitia Iran hadi Uturuki na hatimaye kuzipeleka Ulaya.

Kuhusu suala la maji na haki za maji, Iran inasisitiza kuwa suala hili halihusiani tu na Mto Helmand ndani ya Afghanistan. Ujenzi wa mabwawa kadhaa na serikali ya Taliban kwenye vyanzo vya maji vinavyoelekea Iran pia ni tatizo, na Iran inataka haki zake ziheshimiwe ili upatikanaji wa maji kutoka Afghanistan usizuiliwe.

Ni ukweli usiopingika kwamba uvamizi wa kijeshi wa Marekani nchini Afghanistan ulisababisha mauaji ya maelfu ya watu wasio na hatia na kuathiri vibaya usalama wa nchi hiyo na eneo zima. Pia, uwepo wa wanajeshi wa Marekani ulikuwa sababu kuu ya ongezeko la uzalishaji na usafirishaji wa dawa za kulevya nchini Afghanistan.

Kwa kuzingatia athari mbaya za uingiliaji wa mataifa ya kigeni katika historia ya Afghanistan, chaguo bora kwa viongozi wa nchi hiyo ni kushirikiana na Iran kama jirani, nchi ambayo daima imeonyesha nia njema na kujitolea katika masuala ya kisiasa na kiuchumi.