HRW: Bahrain imewapokonya uraia watu 8 na kuwapeleka Iraq
Katika kile kinachoonekana na muendelezo wa sera kandamizi za Bahrain, utawala wa Aal-Khalifa umewapokonya uraia watu wanane na kuwapeleka nchini Iraq.
Shirika la kutetea haki za binadamu la Human Rights Watch limesema wanane hao ambao walipokonywa uraia mwaka 2012 wamesafirishwa Iraq kupitia mji mtakatifu wa Najaf.
Sarah Leah Whitson, Mkurugenzi wa Human Rights Watch katika eneo la Mashariki ya Kati amekosoa hatua hiyo ya serikali ya Bahrain ya kutumia njia zote za ukandamizaji kuwafumba midomo wapinzani na wakosoaji wake, ikiwemo kuwavua uraia na kuwatimua nchini.
Amesema, "Wabahrain wanaothubutu kuzungumza masuala ya mabadiliko ya uongozi katika nchi yao wapo katika hatari ya kukamatwa na kuzuiliwa, kukandamizwa, kupokonywa uraia na hata kupelekwa katika nchi nyingine wanakokutana na mustakabali wenye kiza."
Itakumbukwa kuwa, Februari mwaka 2011, wananchi wanamapinduzi wa Bahrain walianzisha mwamko mkubwa wa Kiislamu dhidi ya utawala wa ukoo wa Aal-Khalifa na tokea wakati huo maadanmano ya amani yamekuwa yakiendelea takribani kila siku; huku utawala huo ukitumia mkono wa chuma kuwakandamiza wananchi.