Iraq: Saudia ilikuwa inawaruhusu magaidi kuingai nchini mwetu kuchafua usalama
Wizara ya Ulinzi ya Iraq imetoa taarifa ikisema kuwa, utawala wa Aal-Saud nchini Saudia kuanzia mwaka 2004 hadi 2016, ilipuuza suala la kuwazuia magaidi wa Kiwahabi na wakufurishaji kuingia katika ardhi ya Iraq na kuchafua usalama.
Kadhalika Wizara hiyo ya Ulinzi ya Iraq imesema kuwa, mbali na Saudia kutowazuia magaidi hao kuingia nchini humo, pia haikusaidia kutoa taarifa muhimu kuhusu magaidi waliokuwa wanaingia Iraq iwe ni kutokea Syria au kuingia moja kwa moja kutokea Saudia.
Mtandao wa habari wa al-Arabi al-Jadid umemnukuu afisa wa ngazi ya juu wa Iraq ambaye hakutaka kutaja jina lake akisema kuwa, kwa mujibu wa ripoti iliyotolewa na Wizara ya Ulinzi ya Iraq, Riyadh ilikusudia kuchafua usalama wa taifa la Iraq kwa shari ya magaidi hao. Afisa huyo ameongeza kuwa, katika miezi mitatu ya hivi karibuni uingiaji wa magaidi hao umepungua sana ambapo kinyume chake magaidi hao wamezidi kuingia nchi za Ulaya na Kiarabu, baada ya kushindwa vikali na majeshi ya Iraq na Syria.
Kwa mara kadhaa viongozi na shakhsia mbalimbali wa Iraq wamekuwa wakiikosoa Saudia kutokana na mienendo yake hasi na ya chuki katika kuyaunga mkono makundi ya kigaidi kwa silaha na fedha chini ya muungano wa Marekani na madola mengine ya Magharibi. Katika taarifa nyingine, jeshi la Iraq limefanikiwa kuzuia shambulizi la wabeba silaha waliojaribu kuvamia kituo kimoja cha polisi katika mji wa al-Ramadi, makao makuu ya mkoa wa al-Anbar, magharibi mwa Iraq.