Oman yahimiza kuungwa mkono haki za wananchi wa Palestina
Waziri wa Mambo ya Nje wa Oman ameyahimiza mataifa ya dunia kuunga mkono haki za wananchi wa Palestina na mapambano yao hadi watakapopata ushindi na uhuru wao.
Yusuf bin Alawi, alisema hayo jana Jumanne wakati alipoonana na Jibril al Rajoub, katibu wa kamati kuu ya harakati ya Fat'h ya Palestina mjini Muscat, Oman. Alisema: Utatuzi usiokwenda sambamba na sheria na maazimio ya kimataifa na makubaliano yaliyotiwa saini baina ya Ramallah na Tel Aviv, hauwezi kukubaliwa na Oman.
Amesema, njia yoyote ya kutatua mgogoro wa Palestina inabidi uheshimu suala la kuundwa nchi huru ya Palestina katika mipaka wa tarehe 4 Juni 1967 mji mkuu wake ukiwa ni Baytul Muqaddas Mashariki.
Kwa upande wake Jibril al Rajoub, katibu wa kamati kuu ya harakati ya Fat'h ya Palestina ameishukuru Oman kwa msimamo wake thabiti wa kuunga mkono haki za wananchi wa Paelstina hadi watakapopata uhuru wao na kuundwa nchi huru ya Palestina baada ya kukombolewa ardhi yao kutoka katika makuchana ya Israel.
Vile vile amempa maelezo mafupi Waziri wa Mambo ya Nje wa Oman kuhusu matukio ya hivi karibuni kabisa ya Palestina kama vile suala la umoja wa kitaifa baina ya makundi ya Palestina na utangulizi wa kuundwa baraza la taifa zima la Palestina.