UN: Israel imebomoa nyumba 197 za Wapalestina Ukingo wa Magharibi
Ofisi ya Umoja wa Mataifa ya Kuratibu Masuala ya Kibinadamu (OCHA) imesema utawala wa Kizayuni wa Israel umebomoa nyumba 197 za Wapalestina katika Ukingo wa Magharibi wa Mto Jordan katika miezi mitatu ya kwanza ya mwaka huu wa 2018.
Hayo yanaripotiwa huku utawala huo ghasibu wa Israel ukiendeleza sera zake za kupora ardhi za Wapalestina.
Katika taarifa yake siku ya Jumatano, OCHA imesema mwezi ulipotia pia nyumba zingine 10 za Wapalestina zilibomolewa mwezi uliopita katika eneo hilo la Ukingo wa Magharibi.
Hali kadhalika OCHA imesema bomoa bomoa hiyo ya nyumba za Wapalestina imeongezeka kwa asilimia 12 katika mji wa Quds Mashariki katika robo ya kwanza ya mwaka huu ikilinganishwa na wakati mshabaha mwaka jana. Bomoa bomoa hiyo ilishika kasi Disemba mwaka jana wakati Rais Donald Trump wa Marekani alipotangaza Quds Tukufu kuwa mji mkuu wa utawala bandia wa Israel.
Utawala haramu wa Israel unabomoa nyumba za Wapalestina na kujenga mahala pake vitongoji vya walowezi wa Kizayuni kinyume na sheria za kimataifa.
Itakumbukwa kuwa tarehe 23 Desemba mwaka uliopita wa 2016, Baraza la Usalama la Umoja wa Mataifa lilipitisha azimio linalotaka kukomeshwa ujenzi wa vitongoji vya walowezi wa Kizayuni katika ardhi za Palestina zinazokaliwa kwa mabavu