Paris: Upo uwezekano wa kuiwekea vikwazo Saudi Arabia
Waziri wa Mambo ya Nje wa Ufaransa amesema kuwa upo uwezekano Saudia ikawekewa vikwazo iwapo itakuwa imehusika katika mauaji ya mwandishi wa habari mkosoaji wa utawala wa ukoo wa Aal Saud, Jamal Khashoggi.
Jean- Yves Le Drian amesema kuwa serikali ya Ufaransa itachukua hatua za lazima dhidi ya wale wote waliohusika na mauaji ya mwandishi wa habari Jamal Khashoggi madhali hadi sasa wahusika wa mauaji hayo hawajawekwa wazi na faili lake kutojulikana. Le Drian amesisitiza kuwa, Paris haikanushi uwezekano wa kuwekewa vikwazo Saudi Arabia.
Saudi Arabia ni mnunuzi mkubwa wa silaha, bidhaa za anasa na nyinginezo kutoka Ufaransa. Akijibu swali kuhusu hatua ya Ujerumani ya kusimamisha mauzo yake ya silaha kwa Saudia kutokana na mauaji hayo ya Khashoggi, Waziri wa Mambo ya Nje wa Ufaransa alisema: Berlin imechukua hatua haraka, hata hivyo sisi tunafikiri kuwa tunapaswa kusubiri kukamilika uchunguzi na kujulikana wahusika waliotenda jinai hiyo.
Wakati huo huo Le drian amefichua kuwa kiwango cha uuzaji silaha wa nchi yake kwa Saudia ni cha chini na kudai kuwa Riyadh hununua asilimia 7 tu ya silaha kutoka Ufaransa hivyo Paris haiwategemei Wasaudia katika mauzo ya silaha zake.