Wapalestina kadhaa wauawa shahidi na wanajeshi wa Israel Ukanda wa Gaza
Askari wa jeshi katili la utawala wa Kizayuni wa Israel wamewapiga risasi na kuwaua shahidi Wapalestina wawili katika uzio unaotenganisha Ukanda wa Gaza na ardhi za Palestina zinazokaliwa kwa mabavu na Israel.
Jeshi la Israel limehahalisha ukatili huo kwa kudai kuwa, Wapalestina hao walikuwa wanatega ardhini mada za milipuko mashariki mwa mji wa Khan Yunis mapema leo na ndipo wakauawa kwa kupigwa risasi.
Kwa mujibu wa shirika la habari la Wafa la Palestina, kifaru cha jeshi la utawala huo kimeonekana kikivuka uzio wa Gaza na kukanyaga kikatili miili ya Wapalestina hao waliouawa shahidi. Jana Jumamosi, askari polisi wa utawala huo khabithi walimuua kwa kumpiga risasi Mpalestina mwingine katika mji wa Quds Tukufu, kwa kizingizio kuwa alitaka kumdunga kisu askari wa Israel.
Harakati ya Jihadul Islami ya Palestina imelaani jinai hiyo ya kinyama ya Israel na kusisitiza kuwa, makundi ya muqawama ya Palestina bila shaka yatalipiza kisasi cha damu za Wapalestina wanaouawa shahidi kila uchao na Wazayuni maghasibu.
Kwa mujibu wa Jumuiya ya Taifa ya Familia za Kipalestina, Wapalestina 149 waliuawa shahidi na askari wa utawala haramu wa Israel mwaka uliopita wa 2019, ambapo asilimia 74 miongoni mwao walikuwa wanatoka Ukanda wa Gaza.
Aidha taasisi hiyo ya kutetea haki za Wapalestina imesema kuwa, asilimia 23 ya Wapalestina waliouawa shahidi mwaka jana ni watoto wadogo.