Maafisa wa serikali ya Bahrain waenda kujidhalilisha Israel
Waziri wa Mambo ya Nje wa Bahrain ameongoza ujumbe wa ngazi za juu wa serikali ya Manama kuzitembelea ardhi za Palestina zinazokaliwa kwa mabavu na utawala haramu wa Israel.
Abdullatif bin Rashid Alzayani, Waziri wa Mambo ya Nje wa Bahrain pamoja na maafisa wengine wa utawala huo wa kifalme wameenda Tel Aviv kwa mara ya kwanza kwa kutumia ndege ya abiria ya Gulf Air, na wanatazamiwa kukutana na kufanya mazungumzo na Waziri Mkuu wa utawala wa Kizayuni, Benjamin Netanyahu.
Kadhalika Waziri wa Mambo ya Nje wa Marekani, Mike Pompeo anatazamiwa kuwasili Tel Aviv leo Jumatano kwa ajili ya kushiriki mkutano huo wa pande tatu, utakaofanyika katika mji mtukufu wa Quds unaokaliwa kwa mabavu.
Mwezi uliopita, wananchi wenye hasira nchini Bahrain waliandamana kupinga safari ya ujumbe wa Marekani-Kizayuni katika nchi yao kwa lengo la kutangaza rasmi mapatano ya kuanzishwa uhusiano wa kawaida kati ya Bahrain na utawala wa Kizayuni wa Israel.
Tarehe 15 Septemba mwaka huu, Mawaziri wa Mashauri ya Kigeni wa Umoja wa Falme za Kiarabu (UAE) na Bahrain walitia saini makubaliano ya kutangaza uhusiano wa kawaida baina ya nchi zao na utawala ghasibu wa Israel.
Sherehe hizo zilizofanyika katika Ikulu ya Marekani, White House, zilihudhuriwa pia na rais wa Marekani, Donald Trump na Benjamin Netanyahu, Waziri Mkuu wa utawala dhalimu wa Israel.