Sheikh Isa Qassim: Bahrain ni jela kubwa
-
Sheikh Isa Qassim
Kiongozi wa Harakati ya Kiislamu nchini Bahrain amesema kuwa dhulma na ukandamizaji unaofanywa na utawala wa ukoo wa Aal Khalifa dhidi ya taifa la Bahrain umeifanya nchi hiyo kuwa sawa na jela kubwa.
Taarifa iliyotolewa na Ayatullah Sheikh Isa Qassim imesema kuwa, jela kubwa ya Bahrain imejaa magereza na jela ndogo ndogo ambazo mahabusu na wafungwa wake wameswekwa jela kwa sababu tu ya kupinga siasa za utawala wa kiimla.
Sheikh Isa Qassim ameongeza kuwa, kuna ulazima wa kusikilizwa sauti ya wananchi wa Bahrain kwa ajili ya kuainisha mustakbali wa nchi yao na kuheshimiwa matakwa na irada yao; kwani utawala wowote hauwezi kubakia madarakani bila ya kutilia maanani matakwa ya wananchi.
Bahrain ilitumbukia katika hali ya ghasia na machafuko tangu mwaka 2011 kutokana na malalamiko ya wananchi wanaopinga siasa za utawala wa kizazi cha Aal Khalifa.
Asasi za kutetea haki za binadamu zimekuwa zikiulaumu utawala wa Bahrain kwa kuwakandamiza wapinzani na zimetoa wito wa kufanyika marekebisho katika mfumo wa kisiasa wa nchi hiyo.