Wanamichezo wa Jordan wasusia mashindano yaliyowashirikisha Wazayuni
Makundi yanayoliunga mkono taifa la Palestina huko Jordan yamepongeza hatua ya wanamichezo wa nchi hiyo na nyingine za Kiarabu ya kukataa kushiriki mashindano ya magari ya Baja Rally ya Jordan kutokana na waanndaaji wa mashindano hayo kuwashirikisha pia Waisraeli.
Wajordan wamepongeza wanamichezo hao wakisisitiza kuwa, mashindano hayo yaliyofanyika kati ya Alkhamisi na Ijumaa iliyopita ni sehemu ya sera za kuanzisha 'uhusiano wa kitamaduni' na utawala wa Kizayuni wa Israel.
Mashirika yanayomfadhili bingwa wa mchezo huo raia wa Jordan, Saif Al-Abadi, wamempongeza mwanamichezo huyo kwa hatua yake ya kujiweka mbali na mashindano hayo kutokana na ushiriki wa Wazayuni.
Mashirika hayo ya kibiashara ya Jordan yamesema hatua yao hiyo ya kumtaka Al-Abadi asusie mashindano hayo inatokana na msimamo wao wa kuwaunga mkono wananchi wa Palestina.
Wananchi wa Jordan wametumia mitandao ya kijamii kulaani hatua yoyote ile ya kutaka kuanzisha uhusiano wa kawaida na utawala ghasibu wa Israel.

Aidha wametumia majukwaa hayo kuwapongeza wanamichezo wa nchi yao kwa kususia mashindano hayo ya magari ya Baja ambayo Wazayuni 13 walishiriki.
Mara kwa mara, wananchi wa Jordan wamekuwa wakiandamana wakilalamikia mwenendo wa baadhi ya mataifa ya Kiarabu wa kuanzisha uhusiano wa kawaida na utawala haramu wa Israel unaotenda jinai kila uchao dhidi ya wananchi madhulumu wa Palestina.