Ngao ya ulinzi ya Syria yatungua makombora ya Israel Damascus
Kikosi cha Ulinzi wa Anga cha Jeshi la Syria kimetangaza kutungua makombora yaliyovurumishwa na utawala haramu wa Israel kuelekea viungani mwa mji mkuu Damascus.
Shirika rasmi la habari la Syria SANA limetangaza kuwa, usiku wa kuamkia leo Jumatatu, ngao ya ulinzi wa anga ya Syria ilitungua makombora hayo ya Israel ambayo yalikuwa yamevurumishwa kutoka Milima ya Golan ya Syria inayokaliwa kwa mabavu na utawala huo pandikizi.
Duru za kijeshi zimeiambia kanali ya Press TV kuwa, "Ngao zetu zimetungua makombora ya wavamizi. Shambulizi hilo halijasababisha maafa ghairi ya uharibifu mdogo."
Jeshi la utawala dhalimu wa Israel limekuwa likivurumisha makombora mara kwa mara nchini Syria lakini makombora mengi hutunguliwa na vikosi vya ulinzi wa anga vya nchi hiyo ya Kiarabu.
Mara kwa mara, Syria imekuwa ikilaani mashambulio ya utawala wa Israeli katika ardhi yake ikisema vitendo hivyo vya uchokozi vya Tel Aviv havitaathiri azma ya nchi hiyo ya Kiarabu katika vita dhidi ya ugaidi.
Utawala haramu wa Israel ni muungaji mkono mkubwa wa magaidi ambao wanataka kuiangusha serikali halali ya Rais Bashar al Assad nchini Syria.