Maandamano dhidi ya Trump na Musk kila siku Washington DC
https://parstoday.ir/sw/news/world-i123814-maandamano_dhidi_ya_trump_na_musk_kila_siku_washington_dc
Mji mkuu wa Marekani, Washington DC, unaendelea kushuhudia maandamano ya karibu kila siku dhidi ya Rais Donald Trump kutokana na hatua zake za kuwaachisha kazi wafanyakazi, kubana matumizi  na kusaini maagizo ya kiutendaji ambayo yanakiuka maslahi ya nchi.
(last modified 2025-03-12T08:23:55+00:00 )
Mar 12, 2025 08:23 UTC
  • Maandamano dhidi ya Trump na Musk kila siku Washington DC

Mji mkuu wa Marekani, Washington DC, unaendelea kushuhudia maandamano ya karibu kila siku dhidi ya Rais Donald Trump kutokana na hatua zake za kuwaachisha kazi wafanyakazi, kubana matumizi  na kusaini maagizo ya kiutendaji ambayo yanakiuka maslahi ya nchi.

Washington DC, eneo la saba kwa ukubwa wa miji nchini ndilo lililoathirika  zaidi na hatua hizo za Trump, huku wakazi wa Washington DC wakiwa hawana wa kuwatetea, kwani hawaruhusiwi kuwa na uwakilishi wowote ndani ya Bunge la Congress.

Washington DC ina karibu asilimia 45 ya wafanyakazi wote walioajiriwa na serikali ya shirikisho

Maandamano dhidi ya Idara ya Ufanisi wa Serikali (DOGE) hasa yanafanyika karibu kila siku kwa sababu Trump amemteua tajiri mwenye utata, yaani Elon Musk, kusimamia taasisi hiyo. Musk ameibua hasira miongoni mwa Wamarekani  hasa wafuasi wa chama cha upinzani cha Democrat.

Masoko ya fedha ya taifa yameshuhudia hali mbaya zaidi tangu janga la COVID-19, huku hali ya stagflation – mchanganyiko wa mdororo wa uchumi na mfumuko wa bei – ikionekana kuwa jambo la uhakika katika siku zijazo, wakati muhula wa pili wa Trump unaendelea kugawanya taifa.

Trump alitangaza Jumanne kuwa ghasia dhidi ya maduka ya Tesla zitachukuliwa kama ugaidi wa ndani, na wahusika "watapitia jahannamu," akionyesha mshikamano wake na Mkurugenzi Mkuu wa kampuni hiyo ya magari ya umeme, mshirika wake Elon Musk.

Msemaji wa White House, Harrison Fields, amesema kuwa “matukio ya ghasia dhidi ya Tesla yanayofanywa na wanaharakati wa mrengo wa kushoto si chochote bali ni ugaidi wa ndani.”