Putin: Tuko tayari kupigana na Ulaya kama itataka vita
-
Vladimir Putin
Rais wa Russia, Vladimir Putin, ameishambulia vikali Ulaya katika matamshi yake ya jana Jumanne, akitangaza utayarifu wa nchi yake kupigana vita dhidi Ulaya, anayoituhumu kuwa inafanya jitihada za kuharibu makubaliano ya kusimamisha mapigano nchini Ukraine na kuishinda Russia kistratijia.
Putin ametoa matamshi hayo mjini Moscow kabla ya mazungumzo yake tarajiwa na mjumbe wa Marekani, Steve Wittkopf na mkwe wa Donald Trump, Jared Kushner. Amesema: "Kama Ulaya inataka kuanzisha vita vya ghafla nasi na ikafanya hivyo, inaweza kujitokeza hali ya haraka sana ambapo hatutakuwa tena na mtu wa kujadiliana naye."
"Hatuna nia ya kupigana vita na Ulaya; tayari nimesema hivyo mara 100. Lakini kama Ulaya inataka ghafla kupigana vita dhidi yetu na kuvianzisha, tuko tayari hivi sasa. Hakuna shaka kuhusu hilo", amesisitiza Rais wa Russia.
Putin amesema kwamba Ulaya "inasimama upande wa vita na haina ajenda ya amani," akieleza kuwa nchi za Ulaya zinatoa mapendekezo yasiyokubalika kwa Russia kuhusu suluhisho la amani nchini Ukraine.
Putin amesema kwamba Ulaya "inaendelea kuishi katika ndoto za kuishinda Russia kimkakati, na imekata mawasiliano na Moscow kwa hiari yake yenyewe."