Putin: Vikwazo vya Marekani na Ulaya dhidi ya Russia, vitawadhuru wenyewe
-
Rais Vladimir Putin wa Russia
Rais Vladmir Putin wa Russia amesema kuwa, vikwazo vya Marekani na madola ya Magharibi dhidi ya nchi yake, vitakuwa na madhara kwa mataifa hayo yenyewe.
Rais Putin amesema kuwa, vikwazo hivyo dhidi ya Russia, vitakuwa na madhara makubwa kwa uchumi wa Marekani na Ulaya. Amefafanua kuwa, huko nyuma Moscow ilifanya juhudi kubwa za kuishawishi Marekani ishirikiane nayo katika uga wa mapambano ya kimtandao (Cyber), hata hivyo Marekani haikuwa tayari kushirikiana na Russia katika suala hilo.
Kwa mujibu wa Rais Vladmir Putin wa Russia, Moscow haikuhusika hata kidogo katika kuingilia uchaguzi wa rais wa mwaka jana nchini Marekani. Amesisitiza kuwa, binafsi yupo tayari kukutana na Rais Donald Trump kwa ajili ya utatuzi wa tofauti zilizopo hivi sasa baina ya Moscow na Washington.
Uhusiano wa Marekani na Russia umeharibika katika miaka ya hivi karibuni kufuatia mgogoro wa Ukraine na kadhalika madai ya viongozi wa Washington kwamba Moscow iliingilia uchaguzi wa Marekani na kumuingiza madarakani Rais Trump, suala ambalo linakadhibishwa na Russia.
Hivi karibuni bunge la Russia liliunga mkono pendekezo la kufanyika uchunguzi kuhusu vyombo vya habari vya Marekani vinavyofanya kazi huko Russia. Uchunguzi huo ambao utafanywa na kamati ya teknolojia, habari na mawasiliano ya bunge la Russia, utachunguza swali kwamba je kanali ya CNN, Sauti ya America, Redio Uhuru na vyombo vingine vya habari vya Marekani vinafanya kazi kwa mujibu wa sheria za Russia au la?