Malaysia yasema magaidi 34 wa nchi hiyo wameangamizwa Iraq na Syria
Naibu Waziri wa Mambo ya Ndani wa Malaysia amesema kuwa, kwa akali magaidi 34 wenye uraia wa taifa hilo wameangamizwa nchini Iraq na Syria.
Ahmad Zahid Hamidi amesema kuwa kati ya magaidi 346 waliotambuliwa kujihusisha na makundi ya kigaidi na ambao ni raia wa nchi hiyo 34 wameangamizwa. Aidha amefafanua kuwa, magaidi hao waliouawa ni kati ya magaidi 53 ambao walikuwa wakishirikiana na magaidi nchini Iraq na Syria. Amesisitiza kuwa, vitisho vya kigaidi nchini Malaysia vimekomeshwa kutokana na msaada wa polisi ya kimataifa (Interpol) na mashirika mengine ya upelelezi ya kimataifa.
Kwa mujibu wa ripoti, tangu mwanzoni mwa mwaka 2017 hadi sasa, maafisa wa usalama wa Malaysia wamefanikiwa kuwanasa magaidi 45 wenye uraia wa kigeni ndani ya mipaka ya nchi hiyo. Magaidi hao waliotiwa mbaroni ni raia wa Indonesia, Ufilipino, Uturuki, Iraq na Yemen. Inafaa kuashiria kuwa, tangu kulipoibuka mgogoro wa Syria mwaka 2011, magaidi wenye kufuata idolojia ya Uwahabi kutoka nchi mbalimbali za dunia walitumwa nchini humo na nchi za Marekani na Saudia kwa lengo la kutaka kuiondoa madarakani serikali halali ya Damascus, njama ambazo hata hivyo zimeambulia patupu.